Tuesday 21 March 2017

NAIBU WAZIRI TAMISEMI, SULEIMAN JAFO AMUAGIZA MKANDARASI ANAYEJENGA BARABARA WILAYANI RUANGWA KUZINGATIA UBORA NA THAMANI YA FEDHA ZA UJENZI


Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mh. Selemani Jaffo akiwa anatoa maelekezo kwa Mkurugenzi wakati alivyotembelea shule mpya
Mh Naibu Waziri Mhe.Selemani Jafo akiwa anazungumza na Watumishi wa Ruangwa katika ukumbi wa CWT(kulia)Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi Ramahani Kaswa(kushoto)Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Joseph Mkirikiti
Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa pamoja na timu ya Usalama Wilaya wakiwa wanamsikiliza Naibu Waziri Mhe. Jafo alipokuwa anazungumza na Watumishi hao
Naibu Waziri Jafo akiwa anakagua ujenzi wa wodi mbili zinazijengwa katika hospitali ya Nadangala(kulia) Kaimu Mganga Mkuu Peter Mnyale  (kushoto) Mkuu wa Wilaya Mhe. Joseph Mkirikiti
Barabara ya Nachingwea ikiwa katika hatua za mwanzo za ujenzi wa lami

Na: Mwanakheri Ally

Naibu Waziri TAMISEMI Mhe. Suleimani Jafo amemtaka mkandarasi anaemiliki Kampuni ya Wanyumbani Construction anayejenga barabara za lami katika Wilaya ya Ruangwa kujenga barabara hizo katika kiwango cha ubora unaotakiwa na kwa muda uliopangwa.

Pia amemtaka Mkadarasi huyo kutumia malighafi za ujenzi zilizokusudiwa ili kuweza kufanikiwa kuwa na barabara zenye ubora uliokusidiwa na zitakazodumu muda mrefu.

Mhe. Jafo ameyasema hayo wakati akikagua barabara za lami zinazojengwa na mkadarasi mwenye Kampuni ya Wanyumbani Construction wakati wa ziara yake ya kikazi iliyofanyika katika Wilaya ya Ruangwa.

Aidha, Naibu Waziri huyo alimtaka Mkurungezi wa Halmshauri ya Wilaya ya Ruangwa Ndugu Andrea Chezue kuendelea kufuatilia kwa ukaribu ujenzi wa vyumba vya madarasa ya shule mpya inayojengwa Wilayani hapo ili shule hiyo iweze kuwa na ubora.

“kwa kuangalia jinsi majengo yalivyo, inaonesha kabisa majengo haya yana ubora unaotakiwa hivyo hongereni sana na hongera zaidi kwa Mbunge wa Jimbo kwa msaada alioutoa na anaoendelea kuutoa katika ujenzi wa shule hiyo” alisema

Wakati huo huo Naibu Waziri Jaffo amewataka Watumishi wa Wilaya ya Ruangwa kuacha kufanya kazi kwa mazoea na kuanza kufanya kazi kwa bidii ili kufikia kasi inayotakiwa.

Alisema Naibu Waziri Watumishi wa Ruangwa wanapaswa kuwa mfano wa kuingwa katika Wilaya nyingine kwani wanapaswa kufanya kazi kwa bidii ili wasimuangushe Waziri Mkuu.

“Msijibweteke na msifanye kazi kwa mazoea huu ni wakati wa kubadilika na kuwa Watu wapya kama ujabadilika basi fanya kubadilika mara moja ili uweze kuendana na kasi ya Rais John Pombe Magufuli” alisema.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Mhe.Joseph Mkirikiti aliwataka Watumishi kuzingatia maagizo ya Naibu Waziri na kuyafanyia kazi kwani ni wajibu wa kila Mtumishi kufanya kazi kwa bidii na kufuata taratibu za kiutumishi. 

Aidha alimuahidi Naibu Waziri kutekeleza maagizo yote aliyoyatoa na kuyatafutia ufumbuzi kama inavyotakiwa mara moja.