Monday 26 December 2016

MKUU WA MKOA WA LINDI APIGA MARUFUKU MATUMIZI MABAYA YA CHAKULA KWENYE SHEREHE ZA KIMILA

Na: Mwanakheri Ahmed
Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Godfrey Zambi amepiga marufuku kufanyika kwa shughuli zozote zile za kimila zinazotumia chakula kuanzia mwezi wa huu wa Disemba mpaka Mei 2017.

Shughuli hizo ni pamoja na Unyago, Ndoa na Ngoma za Majini. Alisema shughuli hizo zinazofanywa na Wananchi zimekuwa zinatumia chakula kingi hali hii inaweza kupelekea kutokea kwa janga la njaa mkoani hapo.

Mkuu huyo wa Mkoa wa Lindi aliwataka Wananchi kuwa wavumilivu na waelewa kwani janga la njaa halichagui Mkoa bali matumizi mabovu ya chakula yanaweza kuleta janga hilo kwa Wananchi wote.

“Sitaki kuwa Mkuu wa Mkoa ambaye Mkoa wangu umekutwa  na janga la njaa kwani hii ni aibu kubwa hivyo Watu wawe makini katika matumizi ya chakula hata kama chakula wanalima kwa nguvu zao wenyewe".

Wakati huo huo Mhe. Zambi aliwataka Wananchi  wa Ruangwa wajenge vyoo imara na vya matumizi ya muda mrefu, ili kuweza kujiepusha na maradhi ya Kipindupindu kama ambavyo yanaikabili Wilaya ya Kilwa.

Aidha, Mkuu wa Mkoa aliwataka Watendaji wa vijiji kusimamia zoezi la kila Mwananchi wa eneo lake anakuwa na choo imara na Mtu atakaekaidi kufanya ujenzi wa choo cha nyumbani kwake basi achukuliwe hatua za kisheria.

Vilevile aliwasa Wananchi kuwa na matumizi mazuri ya pesa wanazoipata za kuuza korosho au fidia wanazolipwa na kuacha matumizi mabovu ya pesa hizo kama ambaVyo inafanywa na baadhi ya Watu.

Mhe. Zambi aliwakata Wananchi kutumia pesa wanazozipata katika kutengeneza maisha yao kama katika kusomesha Vijana wao na kujenga nyumba imara kwa ajili ya familia zao.


Mkuu wa Mkoa Godfrey Zambi akiwa anaongea na wanakijiji wa Kijiji cha Makanjiro











Mkuu Wa Wilaya ya Ruangwa Joseph Mkirikiti akiwa anaongea na wananchi wa kijiji cha Mandawa